Showing posts with label Communication. Show all posts
Showing posts with label Communication. Show all posts

Monday, September 11, 2017

NAFASI YA MAZUNGUMZO YAKO KATIKA UTASHI WAKO WA KIHISIA

Je wajua kuwa mazungumzo yako ni kipimo cha utashi wako wa kihisia? Je wajua ya kwamba mazungumzo yako yana mchango katika uimara wa utashi wako wa kihisia. Jiulize tu swali moja, unazungumza nini?

Mfumo wako wa mazungumzo au uwasilishaji mawazo yako ni kipimo cha utashi wako wa kihisia. Jinsi unavozungumza juu ya maswala yenye miguso ya kihisia ndivo jinsi utashi wako wa kihisia ulivo. Watu wengi hudhani kuwa uhuru wa kuzungumza katika kutoa mitazamo ya kihisia ni sawa na uhuru wa kuzungumza katika maswala ya kiakili na kifikra, hapana. Uhuru wa kihisia unahitaji mguso wa kinafsi na ufahamu wa aina ya utu wa nafsi husika.

Watu wengi wamejikuta wanazungumza katika lugha hasi yenye harufu ya ukosefu wa imani na ladha ya uchungu wa maumivu kwakuwa ndivo utashi wao wa kihisia ulivo. Wengi wanazungumza nyuma ya pazia la woga na hofu wakionekana ni watu wenye uimara mkubwa kifikra kumbe kihisia ni nafsi ambazo zina hofu hata ya kupatwa na mawimbi ya kihisia. Ukiweza tambua miundo ya lugha na mitazamo utatambua kuwa kuna changamoto kubwa katika utashi wa kihisia.

Tambua ya kwamba kimjazacho mtu ndicho kimtokacho. Inatakiwa tutambue ni nini haswa hutujaza nafsi zetu. Kuna mazungumzo tunayopenda kuyapa nafasi pengine kwa utamu wake  wa kimaudhui wenye kuburudisha nafsi zenye shauku ya kutaka ufahamu pengine hata kama maudhui haina tija wala faida lakini mazungumzo hayo ndiyo yanajaza nafsi zetu magugu yanayoenda kusababisha udhaifu wa kihisia. Shauku isiyo na nidhamu ni adhabu kwa hisia na nafsi. Lazima ujifunze kuratibu mazumgumzo.

Kuna mazungumzo pia tunayofanya ambayo hutudhoofisha nafsi zetu na kutupa misukosuko ya kihisia isiyo na tija. Hivo ni muhimu kutambua na kufahamu aina ya mazungumzo na mguso wake kwa hisia zako

Hatuwezi kuwa watu wenye nafsi imara na utashi wa kihisia bila kuwa watu wenye kuratibu aina ya mazungumzo tunayofanya. Ni jambo gumu sana kuwa mtu mwenye mazungumzo yasiyo na tija kuwa na utashi wa kihisia pengine ni rahisi hata ngamia kupenya katika tundu la sindano. Lazima uwe makini na mazungumzo yako.

Ratibu vyema mazungumzo yako ili safari yako ya utashi wa kihisia iweze kuimarika.

Sunday, October 23, 2016

TENGENEZA MKONDO MZURI WA MAWASILIANO

Moja ya changamoto katika maisha ni pale tunaposhindwa kutengeneza mkondo mzuri wa mawasiliano na hii upelekea mikwaruzano na hata hali ya taharuki na hata hali ya mashaka juu ya mustakabali mzima wa mambo.

Mahusiano pasipo mawasiliano mazuri ya kinafsi ni chanzo kikubwa cha huzuni na hata kuumizana, waweza kuwa na nia njema lakini ukishindwa kutengeneza mkondo mzuri wa mawasiliano unaweza eleweka vibaya. Au unaweza kumuumiza mtu mwingine, ni muhimu sana ukawa mtu wa kuwa unazungumza.

Ni lazima ujenge hali nzuri na msingi imara ili uweze kuwasiliana na mwenzako au yule ambaye unataka kuwasilisha kile unachoona kinakutatiza. Wakati mwingi huwa tunadhani kwamba ni lazima tutafute misamiati mizuri ya mawasiliano, ni kweli pia kuna wakati unaweza kuwasilisha jambo fulani likapokelewa usivyodhania ndo maana kuna wakati unaweza kuwa na hofu fulani.

Ni muhimu kujenga msingi wa uwazi na ukweli na uwe huru maana pasipo uhuru wa nafsi juu ya jambo fulani huwezi kujenga mkondo mzuri wa mawasiliano ndio maana ni muhimu kuwa na msingi mzuri wa kihisia ukitaka kuwa na mkondo mzuri wa mawasiliano...Tambua ya kwamba unapokuwa huru kuzungumza ndio utakuwa na uhuru wa kuwa vile unavotaka.

Kuna sauti nyingi ambazo zinaweza kuja katika akili yako kukuzuia kujenga mkondo mzuri wa mawasiliano, kukosa amani ya nafsi, hofu au hata kutotaka kufikiriwa au kutazamiwa vibaya ndio maana inakupasa uwe na uhuru na amani ya nafsi na utambue kuwa wewe ni nafsi huru na unatakiwa uwe huru kuwasilisha yaliyo katika nafsi yako.

Jifunze kuzungumza kama unadhani huwezi kuzungumza yaliyo ndani ya nafsi yako, tambua nafsi yako ina uzuri na ukuu ambao kama ukishindwa kuzungumza inakuwa vigumu kueleweka....iache nuru yako ing'ae...usihofie kuzungumza. Usipozungumza unaweza jikuta upo katika hali ya taharuki na ukaishi kama mfungwa wakati ukisema ukweli utakuwa huru

Hekima ni kutambua njia na muda muafaka wa kuzungumza lakini mawasiliano ya nafsi ni jambo la msingi sana, yatakuweka huru. Ukitaka sana kufurahisha watu pia inaweza kuwa changamoto yako kuzungumza, pia usipotaka kuwaumiza watu inaweza kuwa changamoto yako kuzungumza lakini ni vyema ukawa huru katika nafsi.