Friday, October 28, 2016

IMANI YAKO HUJENGA KAWAIDA YAKO

Imani mara nyingi hutokana na uzoefu juu ya jambo fulani, uzoefu huo hujiimarisha katika ubongo wako na kutengeneza mfumo wa kisheria ambao utatawala mitazamo yako na utakujengea kawaida yako. Na mara nyingi kawaida hiyo hujenga utamaduni ambao utakusanya mambo ya kuthibitisha na kuendana na utamaduni huo.

Unapojenga imani fulani siku zote imani hiyo huvuta mazingira husika ya kuthibitisha imani hiyo. Mfano unapojenga imani kuwa katika mahusiano jinsia fulani sio ya kuaminika imani hiyo huvuta mazingira hayo, imani hiyo itakuongoza kuchagua watu wasioaminika na hata itakujenga kutafuta mazingira yasio aminifu katika mahusiano yako ili kuthibitisha imani hiyo.

Siku zote akili hujisikia furaha pale inapothibitisha mitazamo yake na malengo yake..ndio maana siku zote ukithibitisha jambo ulilokuwa na wasiwasi nalo hata kama linaumiza akili yako itasema nilijua tu....tafsiri ya neno nilijua ni kuipa thamani akili yako kwa uthibitisho huo na kuijengea thamani kwa imani hiyo.

Ni muhimu utambue kuwa unatakiwa kutafakari sana kabla hujakiweka kitu kama imani yako kwasababu imani hiyo itakutengenezea kawaida yako. Na siku zote kawaida yako ndio ulimwengu wako. Watu wengi wamejijengea kawaida mbaya hadi pale jambo zuri linapokuja wanalikataa na kuliona haliwastahili. Kuna watu wamejijengea kawaida kiasi cha kwamba jaribio lolote la kutoka hapo ni maumivu kwao.

Usijenge msingi wa kiimani ambao unaona kabisa ni asi kwasababu huo msingi utavuta mazingira ya kuthibitisha hayo uliyoyaweka kama sheria. Hakikisha kabla hujaliamini jambo na kuliweka katika akili yako litafakari. Usije kufungwa na kawaida ambayo itakutesa. Mfano mtu anaweza akaja kukwambia yaani mie kila mahusiano yangu naumizwa...unamuuliza je unadhani kwanini....mtu anakwambia mie nadhani nina mkosi au wanaume wote ni wahuni, au wanawake wote hawaaminiki...Tayari kishajenga imani ambayo inavuta mazingira kuthibitisha imani hiyo.

Ni jambo la muhimu sana kuongeza maarifa juu ya jambo usilolijua badala ya kujijengea imani ambazo zitakujengea kawaida yako. Pia ni kubadilisha taswira yako, ni nini hasa unaangalia au ni wapi hasa mtazamo wako ulipo maana taswira siku zote hukutengenezea imani itakayokujengea kawaida itakayovuta mazingira kuthibitisha mambo husika.

Tuesday, October 25, 2016

UTUMIE VEMA MUDA WA KUSUBIRI

Moja ya changamoto katika maisha ni pale ambapo matarajio yetu yanachelewa, pale ambapo unasubiri jambo fulani likamilike. Ni sawa na kupanda mbegu chini ya ardhi na kusubiri mti uchipuke. Muda mwingi tumekuwa tukiona wakati huo ni mrefu na hata kuingiwa na hisia za huzuni na kuchoka pale tunapoona matokeo yamekawia.

Inapaswa ujifunze kuwa wakati wa kusubiri huwa mrefu na wenye uchungu pale ambapo kwa muda huo unasimama katika mambo mengine huku ukisubiria. Hata mkulima huwa akipanda mbegu hakai akisubiria. 

Jizamishe katika mambo uyapendayo hadi usahau kuwa ulikuwa unasubiria jambo fulani.
Subira yenye furaha ni ile subira ambayo unaifanya huku unaendelea kufanya mambo uyapendayo. Hata katika mahusiano yakupasa kuwekeza pia kuhusiana na nafsi yako wakati uko katika mahusiano na mtu mwingine, mahusiano haimaanishi uiache nafsi yako katika ukame ukisubiria muitikio wa nafsi unayohusiana nayo.

Mfano umepanga kukutana na mtu na hajafika huwa unafanya nini huku ukisubiri?, mfano upo katika foleni sehemu huwa unafanya nini ukisubiria?, mfano umeingia katika mgahawa chakula kimechelewa huwa unafanya nini ukisubiria? Dunia haitakiwi kusimama wakati wewe ukisubiria muitikio wa mtu au jambo. Endelea kufurahisha nafsi yako kwa kufanya yale uyapendayo la sivyo utakuwa unaingiwa na huzuni ukiona jambo linachelewa.

Unasubiri jambo gani katika maisha, iwe katika mahusiano au eneo lolote, usisimamishe dunia ya nafsi yako ukisubiria, kuna mambo mengi unaweza kufanya wakati unasubiria kuna vitabu hujasoma, kuna tabia na vipawa unaweza vikuza, kuna marafiki unaweza wasiliana nao, unaweza kwenda kutembea. Kuna mambo mengi nafsi yako ingependa kuyafanya na bado hujayafanya...tumia huo muda.

Jifunze pia kutembea na kitabu kidogo cha kunakiri mambo au yafundishe macho yako kuona uzuri wa mambo yanayokuzunguka, jenga akili ya kudadisi, andika mambo unayoyaona, changamoto mbalimbali, sikiliza audio za kukujenga, waweza enda kusaidia mtu mwingine, tembelea marafiki na jamàa na mzungumze, kuna sehemu unaweza itajika kusubiri muitikio wa jambo fulani, wewe endelea kuishi dunia iliyomo nafsini mwako.

Hata katika mahusiano watu wamekuwa wakilaumiana kwakuwa husubiri miitikio ya watu fulani lakini huchelewa kuitikia, wakati unasubiri waweza fanya mambo mengine, waweza andika mambo yanayokufurahisha katika mahusiano nk, jizamishe katika mambo ya nafsi yako na vipawa vyako, wekeza katika ufahamu wako.

Sunday, October 23, 2016

TENGENEZA MKONDO MZURI WA MAWASILIANO

Moja ya changamoto katika maisha ni pale tunaposhindwa kutengeneza mkondo mzuri wa mawasiliano na hii upelekea mikwaruzano na hata hali ya taharuki na hata hali ya mashaka juu ya mustakabali mzima wa mambo.

Mahusiano pasipo mawasiliano mazuri ya kinafsi ni chanzo kikubwa cha huzuni na hata kuumizana, waweza kuwa na nia njema lakini ukishindwa kutengeneza mkondo mzuri wa mawasiliano unaweza eleweka vibaya. Au unaweza kumuumiza mtu mwingine, ni muhimu sana ukawa mtu wa kuwa unazungumza.

Ni lazima ujenge hali nzuri na msingi imara ili uweze kuwasiliana na mwenzako au yule ambaye unataka kuwasilisha kile unachoona kinakutatiza. Wakati mwingi huwa tunadhani kwamba ni lazima tutafute misamiati mizuri ya mawasiliano, ni kweli pia kuna wakati unaweza kuwasilisha jambo fulani likapokelewa usivyodhania ndo maana kuna wakati unaweza kuwa na hofu fulani.

Ni muhimu kujenga msingi wa uwazi na ukweli na uwe huru maana pasipo uhuru wa nafsi juu ya jambo fulani huwezi kujenga mkondo mzuri wa mawasiliano ndio maana ni muhimu kuwa na msingi mzuri wa kihisia ukitaka kuwa na mkondo mzuri wa mawasiliano...Tambua ya kwamba unapokuwa huru kuzungumza ndio utakuwa na uhuru wa kuwa vile unavotaka.

Kuna sauti nyingi ambazo zinaweza kuja katika akili yako kukuzuia kujenga mkondo mzuri wa mawasiliano, kukosa amani ya nafsi, hofu au hata kutotaka kufikiriwa au kutazamiwa vibaya ndio maana inakupasa uwe na uhuru na amani ya nafsi na utambue kuwa wewe ni nafsi huru na unatakiwa uwe huru kuwasilisha yaliyo katika nafsi yako.

Jifunze kuzungumza kama unadhani huwezi kuzungumza yaliyo ndani ya nafsi yako, tambua nafsi yako ina uzuri na ukuu ambao kama ukishindwa kuzungumza inakuwa vigumu kueleweka....iache nuru yako ing'ae...usihofie kuzungumza. Usipozungumza unaweza jikuta upo katika hali ya taharuki na ukaishi kama mfungwa wakati ukisema ukweli utakuwa huru

Hekima ni kutambua njia na muda muafaka wa kuzungumza lakini mawasiliano ya nafsi ni jambo la msingi sana, yatakuweka huru. Ukitaka sana kufurahisha watu pia inaweza kuwa changamoto yako kuzungumza, pia usipotaka kuwaumiza watu inaweza kuwa changamoto yako kuzungumza lakini ni vyema ukawa huru katika nafsi.

Monday, October 17, 2016

BADILI TASWIRA WAKO

Changamoto kubwa katika maisha ni kuwa na mitazamo mibovu. Taswira uliyonayo juu ya mambo inatokana na hazina uliyoweka moyoni mwako. Jinsi unavowekeza ndani yako ndo jinsi unavojenga taswira nzuri katika maisha yako. Mambo unayoyaona mazito kwako inatokana na nguvu au hazina uliyowekeza ndani yako.

Usipowekeza katika kukua siku zote hautakuwa mtu mwenye taswira nzuri....ukiwa na hazina ndogo au nguvu ndogo ya kiroho siku zote taswira yako itakuwa na tatizo...na ukikosa taswira nzuri utakuwa ni mtu mwenye kulaumu na kuona kama maisha hayakutendei haki. Maisha yapo siku zote lakini wenye nguvu ndio wanaoweza kustahimili hivo wekeza kuwa na nguvu katika nafsi yako.

Chukua kila tatizo linalokuja kwako na ulione kama jiwe la kwenda kiwango kingine. Chukua maumivu na uyaone kama fursa ya kujiimarisha zaidi roho yako. Usilalamike, wewe ni kiongozi wa maisha yako na kila jambo hufuata mkondo unaouweka wewe. Hukuzaliwa umfurahishe kila mtu hivo acha kufungwa katika mawazo au shuruti za watu. Unatakiwa uwe huru.

Ili taswira yako iwe nzuri ibadilishe, unapokuwa unatafuta taswira ya picha na camera lazima uhakikishe picha ya maisha yako unaiweka katika mraba, kuna vitu vya kuondoa katika taswira hiyo, unaweza kubadili umbali nk. Vivyo hivo katika maisha yako ukitaka upate taswira unayoitaka kuna watu inabidi uachane nao, kuna mambo inabidi uachane nayo, kuna vitu inabidi uviondoe katika taswira. Haijalishi vikoje kama unaona havipo katika taswira yako yakupasa uviondoe.

Usipokua, siku zote taswira yako itakuwa ndogo, kuna mambo mengine hujayajua au kuna mambo mengine huyaoni kwasababu huna taswira nzuri na hii hutokana na kutokuwa na hazina na nguvu ndani yako.


Thursday, October 13, 2016

SAUTI TATU KATIKA MAHUSIANO

Mahusiano yetu huguswa na sauti ambazo zinaleta changamoto na ni sauti ambazo zinamchango katika uimara wa mahusiano yako au kuanguka kwa mahusiano yako. Bila sauti hizo kuwa katika uwiano  sawa basi sauti moja ikiizidi nyenzake inaweza sababisha changamoto.

Sauti hizo zimegawanyika katika makundi matatu, ya kwanza ni sauti ya nafsi ; Hii ni sauti ambayo kila mtu anakuwa nayo kiasili nayo ni sauti ya uhuru, furaha na amani. Kila nafsi inataka kuwa katika uhusiano ambapo itakuwa huru na yenye furaha na amani, sauti hii inalia kutoka ndani ya nafsi ya mtu na ndio maana kuna ambao husema kuwa katika uhusiano ambao utakuwa huru na mwenye furaha na amani.

Sauti ya pili ni sauti ya Jamii; hii ni sauti inayotoka katika jamii inayotuzunguka juu ya mahusiano yetu. Hii sauti inaweza ikawa sauti ya wazazi au sauti ya malezi na makuzi ambayo tumeyapitia. Sauti hii mara nyingi hutuambia kuwa ni nani anatufaa, au ni nani tunatakiwa tuwe naye au ni mahusiano gani ambayo inabidi tuwe nayo.

Sauti ya tatu ni sauti ya akili zetu; Binadamu huwa na hali ya kupenda kutafakari na kutumia akili katika kufanya maamuzi na pengine kuna wakati hutumia zaidi akili katika mambo fulani juu ya nini hasa jambo sahihi la kufanya.

Ili kujenga uhusiano imara lazima hizi sauti ziwe na uwiano...sauti ya nafsi inabidi iwe kama msingi itakayobeba sauti nyingine zote. Sauti ya nafsi ikizifunika sauti nyingine zote unaweza pelekea kufanya mambo ambayo yanaweza kutokubalika katika jamii na ukajikuta unakosa kabisa ushirikiano na wengine lakini sauti ya jamii ikiizidi sauti ya nafsi utajikuta unaingia katika mahusiano ambayo katika jamii unasifika lakini ndani ya nafsi yako unakosa furaha na unakuwa na upweke ambao jamii haiwezi kukusaidia.

Pia inakupasa sauti ya nafsi iwe na uwiano na sauti ya akili ili akili yako iweze kuwekeza zaidi...maana nafsi na akili zikiwa na uwiano ile amani na furaha hudhiirika katika fikra za ubunifu zaidi katika kuimarisha mahusiano hayo.

Kama unaona sauti ya jamii ni kubwa na inakutisha hakikisha sauti ya nafsi na sauti ya akili vinaungana kuishurutisha sauti ya jamii itulie.

Changamoto na jambo la msingi kwa kila mtu ni kuhakikisha hizo sauti zina uwiano ili kujenga mahusiano imara.


Monday, October 3, 2016

TAMBUA UNACHOTAKA KATIKA MAISHA

Moja ya changamoto kubwa ambayo watu wengi huwa tunayo ni kutofahamu nini tunachotaka au tunachohitaji katika maisha. Watu wengi hudhani wanajua wanachokitaka au wanachokihitaji lakini ukiangalia matendo yao utatambua kuwa wengi hawajui wanachokitaka katika maisha. Usipojua unachotaka katika maisha utakuwa ni mtu wa kuzunguka zunguka kujaribu jaribu kila kitu kuona kina mguso gani kwako.

Kuna dhana nyingi sana ambazo tunazo ju ya yale tunayotaka katika maisha na unaweza ukapewa kila ulichodhani unakitaka kisha ukaja kugundua kuwa bado kuna kitu kingine unachokitaka. Na utakuwa ni mtu usiye na furaha wala amani kwasababu hujui unachokitaka. Pengine hata ukawa mtu mwenye lawama katika kila jambo kwasababu wewe mwenyewe hujui unachokitaka.

Pengine pia unaweza jua unachokitaka lakini unadhani ni jambo la kufikirika, huo mtazamo unaweza kukufanya ukaendelea kuwa kama mtumwa anayezunguka jangwani asijue anapoelekea. Kuna mwanafilosofia mmoja aliwahi kusema kuwa Watu wengi hawajui wanachokitaka hadi uwaonyeshe wanachokitaka. Ni muhimu sana kujua unachokitaka.

Njia pekee ya kujua unachokitaka ni kujitathmini nafsi yako na kujitambua utu wako ndipo utajua ni nini unachohitaji. Mwanafilosofia mmoja aliwahi kusema kuwa kama hakuna adui ndani adui wa nje hawezi kutudhuru. Nafsi yako ya ndani imeundwaje? Pengine ushawahi kujiuliza ni jambo gani linakupa amani na unaamini ndio jambo ambalo ukilipata kama msingi wa maisha yako utaweza kupata mambo mengine yote?

Kila nafsi inahitaji uhuru na amani na furaha na wengi wetu tumedhani tukipata vitu basi nafsi yetu ndo itakuwa imepata inachotaka. Hapana!! Nafsi yako inahitaji kukua na jambo lolote linaloweza kuinyanyua nafsi yako ndilo jambo unalohitaji. Nafsi yako inahitaji thamani na jambo linaloweza kuipa thamani nafsi yako ndilo unalohitaji. Nafsi yako inahitaji amani na jambo lolote linaloweza kukupa amani ya nafsi ndilo unalohitaji.

Ukishajua msingi hasa wa mahitaji ya nafsi yako itakuwezesha kutambua ni nini unachohitaji katika maisha, iwe ni katika uchaguzi wa kazi, iwe ni katika mahusiano au nyanja yeyote ya maisha. Utatambua marafiki wa nafsi yako, utatambua hata mwenzi wa nafsi yako, utatambua hata kusudi la maisha yako.

Saturday, October 1, 2016

USIOGOPE KUKUTANA NA HOFU YAKO

Moja ya changamoto tunazopitia katika maisha ni hofu ya kukutana na hofu zetu na hofu ya mguso utakaotokana na hofu zetu. Huwezi kuwa huru kutoka katika hofu unayohofia kukutana nayo. Siku zote kuwa tayari kukutana na hofu zako na jivike ujasiri wa kuweza kuzidhibiti hofu zako.

Katika maisha lazima uwe na ujasiri wa kusonga mbele na kujua kuwa iko siku utakutana na hofu zako. Lazima ujipange jinsi ya kukabiliana na hofu yako na uwe jasiri maana hofu yako siku zote ndio gereza lako. Kuna wakati katika maisha inakubidi kuvuka daraja lenye kutia hofu kwa ujasiri ukitazamia maono uliyonayo katika maisha.

Amani ya nafsi ikishakaa ndani yako itakupa ujasiri wa kukabiriana na hofu yako ndio maana mwanafilosofia mmoja aliwahi kusema kuwa kama hakuna adui ndani ...adui wa nje haweza kutuathiri. Na hapa anapozungumzia adui sio lazima awe adui anayekupinga bali kuna maadui wa furaha yako na maono makubwa ambao wanaweza kuja kama watu wa karibu wakikushauri au mazingira fulani yakikukwamisha.

Lazima ujivike ujasiri na useme kwa jambo lolote nitasonga mbele na niko tayari kukutana na hofu yangu. Bila kuwa na huo ujasiri hofu yako itaendelea kukuzuia kusonga mbele. Na njia pekee ya kuweza kuishinda hofu yako ni kuwa mkweli kwa nafsi yako, kuwa mkweli kwa kile nafsi yako inataka na pia kuikubali amani iliyo ndani yako maana amani ya nafsi siku zote ni ya msingi sana. Ukisha kuwa mkweli uweke wazi ukweli ulio ndani yako, usiuogope, wala usiogope jinsi watu watakavoupokea huo ukweli.

Njia ya maisha siku zote ni ya kufanya maamuzi na kusonga mbele. Muda wa kukaa kutafakari kwa sababu ya hofu iliyo mbele yako ni kujikwamisha mwenyewe. Songa mbele kama una imani na kweli iliyo ndani yako. Amini tu kwamba kila jambo linafanyika kuwa jema. Maamuzi siku zote hutujenga, pasipo maamuzi tutaendelea kukaa katika hali ya mazoea ambayo pengine yangekuja kutuumiza.
Kuwa jasiri na Hofu zako zitakimbia. Usipokuwa jasiri hofu zako zitaendelea kukufunga sehemu ulipo.