Monday, January 16, 2017

GHARAMA NA KIPIMO CHA UVUMILIVU

Je wajua kila jambo bora huja na gharama ya uvumilivu. Kila jambo unalohitaji katika maisha huja na gharama ya uvumilivu huku ukikua katika nidhamu katika hicho kipindi cha uvumilivu. Kuna wakati unaweza dhani unaishi katika ndoto pale unapozungumza mambo pasipo kuyaona katika uhalisia.

Imani ni kuwa na uhakika wa mambo ambayo unayo katika fikra lakini bado hayajadhiirika. Unaweza omba msitu lakini ukapata mbegu ya msitu na ukaanza kujiuliza hii mbegu naifanyia nini. Unaweza kuwa na maono ya kujenga familia bora yenye kila hitaji muhimu likiwa limekamilika lakini ukajikuta unapata mwenza ambaye amekamilika katika hitaji la kinafsi lakini mahitaji ya kimali bado inakubidi uvumilie pengine hata uwekeze muda zaidi. Ni wewe kutambua kuwa hiyo uliyonayo ni mbegu bora inayohitaji udongo mzuri ili ichipue yale unayohitaji.

Hitaji la nafsi ni changamoto kubwa na wengi wamekuwa wakipata mahitaji mengine lakini wamekuwa wakiishi pasipo kuridhika kwakuwa mahitaji ya kinafsi wamekuwa wakiyakosa. Tambua kuwa kuna nyakati ambazo uvumilivu na imani yako itawekwa katika kipimo ili kuimarika katika uthabiti wa kimaamuzi. Kila jambo huwa zuri kwa muda kama likijengwa juu ya uaminifu, maono na nia thabiti ya kulisababisha lile jambo litokee katika uhalisia wake.

Lazima ufike kipindi ambacho imani yako itakuwa katika kipimo, lazima ifike kipindi utajiuliza je haya mambo ninayoyatazamia ni ndoto tu za mchana au kweli nitakuja kuyathibitisha. Unapofika katika kipindi hicho uimara wako na imani yako na fikra chanya ndizo zitakazokuvusha kuyapata yale unayoyahitaji na kuyatazamia.

Hakuna ndoto kwa mtu mwenye dhamira ya dhati na kila wakati anahangaika kutafuta njia za kutekeleza yale anayoyaona katika maono yake. Bali ni hatma ya muda na uvumilivu wa huyu mtu akisimama imara katika kutegemea yaliyo bora na yale anayoyatazamia. Usijione kuwa mwenye ndoto tu pengine labda unatazamia mambo ambayo kwa sasa huwezi yapata. Tambua kuwa dhamira ya dhati na utayari wa kujitoa huku ukichanganya na uvumilivu ukiendelea kukua kinafsi vitathibitisha ndoto zako na maono yako.

Wednesday, January 11, 2017

WEKEZA KATIKA UIMARA WA NDANI

Nyumba imara ni ile yenye msingi imara. Msingi mara nyingi hufukiwa chini lakini ndio uimara wa jengo zima ulipo. Vivyo hivyo uimara wako kwa mambo yanayoonekana unatokana na uimara wako wa ndani, uimara wa nafsi. Japo nje waweza onekana imara lakini kipimo pekee cha uimara wako wa ndani ni mtikisiko.

Mtikisiko mkubwa utakaopata ni pale ambapo misingi yako ya ndani itatikiswa. Pale ambapo utawekwa katika mazingira ambayo yatakubidi upime mitazamo yako, upime sheria zako, upime utaratibu wako na kuu kuliko yote upime utambulisho wako. Na ndio maana katika kipindi cha mtikisiko unaweza poteza dira ya utambulisho wako, imani yako na hata utaratibu wako.

Mtikisiko unapoingia lazima uingie uzito wakati huo huo inaingia hali ya hamaki na taharuki. Hapo ndipo utajikuta unafanya maamuzi ambayo hayana faida kwako, hapo utajikuta unaingiwa na ukungu katika macho yako ya ndani ya maono yako.

Hali hiyo ni ya kawaida hasa pale unapotoka katika mfumo mmoja kwenda mwingine, kawaida moja kwenda nyingine. Pale unapotaka kuishi mitazamo yako na ndoto zako kwa mkupuo. Pale unapotaka kukimbia kabla hujapasha joto miguu kwa kutembea. Ni vema ukapasha joto miguu yako na kufurahia kabla hujaanza kukimbia.

Uhuru wa nafsi unahitaji nidhamu na maono yaliyo sambamba na uhalisia. Jaribu kwenda kwa utaratibu lakini ukiwa na uharaka wa kifikra kuchukua maamuzi. Kuwa muwazi juu ya hali yako na utafute watu wachache ambao watakuchoma sindano ya hamasa na watakuamini. Ambao wako tayari kusimama na kukupa moyo.

Unaweza kujiimarisha kwa kuendelea kujipa hamasa na kuwa na fikra chanya, ukichukulia kila changamoto kama njia ya kujiimarisha. Usitafute kujipa kisingizio kama unajua unaweza kujiimarisha. Kila wakati ongeza nguvu yako ya ndani kwa kusimama tena hata kama umechoka. Misuli huja kwa kuongeza zaidi, kujiinua zaidi na kuamini ipo siku mambo yatakuwa mazuri.